Kwa mujibu wa idara ya tarjuma ya Shirika la Habari la Hawza, hafla ya kumbukumbu ya mwaka wa kwanza wa Shahidi wa Muqawama Sayyid Hassan Nasrullah ilifanyika katika msikiti mkuu wa mji wa Skardu, Baltistan, Pakistan, kwa kuhudhuriwa kwa hamasa na ari kubwa na ulamaa, watu wa dini na makundi mbalimbali ya wananchi.
Hafla hiyo ya kiroho ilianza kwa kisomo cha baadhi ya aya za Qur’ani Tukufu, kisha kundi la ulamaa na wahadhiri katika hotuba zao, sambamba na kumtukuza shahidi wa muqawama, walisisitiza juu ya kuendelezwa kwa njia na fikra zake.
Hujjatul-Islam Sheikh Habib Sabiri, mmoja wa wahadhiri mashuhuri wa Pakistan, katika hotuba yake alisema: “Sayyid Hassan Nasrullah alikuwa mwiba machoni mwa maadui, na shahada yake imeonesha kwamba shakhsia hazitoweki, bali mawazo na malengo yao hubaki milele.”
Aidha, Hujjatul-Islam Mushtaq Husayn Hakimi, alizitaja fikra za Shahidi wa Muqawama kuwa ni kielelezo bora cha utiifu kwa kiongozi na kushikamana na wilaya. Hujjatul-Islam Muhammad Husayn Ra’isi naye akisisitiza juu ya misingi ya madhehebu ya Ahlul-Bayt (as) alisema: “Msingi wa Ushia ni kuunga mkono waliodhulumiwa na kusimama imara dhidi ya dhalimu.”
Kisha, Hujjatul-Islam Sheikh Muhammad Jawad Hafizi, naibu wa imamu wa Ijumaa wa Skardu, akasema kuwa; shahada ni neema ya juu zaidi na akasema: “Sayyid Hassan Nasrallah alitumia maisha yake katika kuitumikia haki na alichagua shahada kuwa heshima yake kubwa zaidi.”
Katika sehemu ya mwisho ya hafla hiyo, Hujjatul-Islam Sheikh Muhammad Hasan Ja‘fari, imamu wa Ijumaa wa Skardu, katika hotuba yake alisisitiza: “Shahada ya Sayyid wa Muqawama imeamsha dhamiri ya Umma wa Kiislamu na imebeba ujumbe huu kwamba shahada siyo uharibifu, bali ni kudumu na ni maisha ya milele.”
Akaongeza kwa kunukuu maneno ya Amirul-Mu’minin Ali (as): “Shahada ni ushindi wenyewe, lakini kusalimu amri na kurudi nyuma mbele ya maadui ndiko kifo cha kweli.”
Maoni yako